KWA MAWASILIANO ZAIDI: E-mail: yusuf.badi2@gmail.com.

NSSF

TANGAZO

Friday, July 19, 2013

WAZIRI DKT,MUKANGARA AWATAKA VIJANA KUJIUNGA NA VIKUNDI VYA UJASIRIAMALI ILI WAWZE KUJIKWAMUA KIUCHUMI.

Na. Benedict Liwenga-MAELEZO
VIJANA nchini wametakiwa kujiunga na vikundi vya ujasiriamali na Vyama vya kuweka akiba na kukopa (SACCOS) kama njia ya kujipatia mitaji kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao za uzalishaji mali ili waweze kupata mikopo ambayo itawasaidia kujikwamua kimaisha.
Wito huo umetolewa jana na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara wakati akiongea na Vijana wa Kikundi cha  Mambo Safi kilichopo  kata ya Kimara jijini Dar es Salaam.
Waziri Dkt. Mukangara alisema kuwa katika jitihada za kuwawezesha vijana kuendeleza shughuli zao za uzalishaji mali Serikali kupitia mfuko wa maendeleo ya vijana na kwa kushirikina na vyombo vya fedha na wadau wengine itaendelea kuhakikisha kuwa wanatoa  mikopo yenye masharti nafuu kwa wajasiriamali wadogo wadogo.
“Tutaendelea pia kuwahimiza na kuwatayarisha vijana waliomaliza vyuo vikuu na walio nje ya vyuo kuhakikisha  kuwa wanajiunga katika vikundi mbalimbali vya nguvu kazi ili kujiletea maendeleo.
“Kwani katika umri wa ujana, mnaweza kufanya mambo makubwa na mazuri kwa kutumia nguvu mliyonayo, wengi wenu mna uwezo mkubwa wa kufikiri kwa kutumia teknolojia za kisasa na kuchanganua mambo pia mchangamkie fursa mnazokutana nazo kila siku”,  Alisema Dkt Fenella.
Aidha Dkt. Mukangara amewaasa vijana kutii sheria za nchi na kuheshimu vyombo vya dola kwani hakuna nchi yoyote hapa  duniani ambayo chombo chake cha dola kikiguswa itanyamaza.
“Lakini kubwa kabisa ni kujenga na kutunza nidhamu yenu na kutii sheria na vyombo vya Dola ili tuendelee kudumisha amani na kujiletea maendeleo”. Dkt. Fenella alisema.
Akisoma taarifa ya kikundi hicho Phabbian Salvatory ambaye ni Mkurugenzi wa kikundi alisema kuwa  kazi wanazozifanya ni kutoa darasa la  mafunzo ya kila siku ya sanaa za jukwaani,uzalishaji,maadili,mazingira na afya, kuhamasisha na kutoa burudani kwa njia ya matamasha,kongamano na semina.

Kazi zingine ni kuwafikia vijana popote walipo na kubaini kero zilizopo, kutoa mafunzo  ya ujasiriamali,afya,mazingira,maadili kwa rika tofauti na kujitolea kwa shughuli tofauti za kijamii na Serikalini pale wanapohitajika.

Salvatory alizitaja changamoto zinazowakabili kuwa ni pamoja na kufanya kazi katika mazingira magumu  ya ukosefu wa fedha na vitendea kazi , kudharauliwa na jamii inayowazunguka kuwa sanaa ni uhuni, ukosefu wa mtaalamu wa kuandika miradi, kutokuwa  na mwanasheria wa kusimamia kazi zao kisheria na  ugumu wa vijana katika mapokeo ya shuhguli  tunatozozifanya.

“Pia tunakabiliwa na changamoto ya vijana kukosa subira na mtazamo potofu, ahadi hewa zinazotolewa na viongozi pasipo kutekeleza kwa wakati , kutokupewa fursa zilizoko serikalini  za kitaifa na kimataifa ambako kunapelekea vijana wengi kukata tamaa na kuondoka katika taasisi kwani maisha yao wanategemea hapa na kazi zetu kudhulumiwa na watu mbalimbali.

Waziri Mukangara alitoa zawadi ya Mashine moja ya kutolea kopi aina ya Kyocera, Kompyuta Mpakato (Laptop) moja aina ya Samsung, Mipira 22 kwa kikundi hicho  pia alitoa zawadi  ya Jezi seti mbili na Mipira 2 kwa vijana wa Mabibo jijini Dar es Salaam, vitu vyote hivyo  vinathamani ya shilingi  Milioni 3.7.
Kikundi cha mambo safi kilichosajiliwa  kisheria  na baraza la sanaa la taifa (BASATA) mwaka 2008 kwa ajili ya kuendesha shughuli za vijana na uchumi ,sanaa,michezo na maendeleo ya  jamii.

No comments: