Anna Nkinda – Maelezo, aliyekuwa Mbeya
Taasisi ya Wanawake na Maendelea (WAMA) imetoa msaada wa 
cherehani ya kudarizi kwa mjane Fatma Almasi ambaye ni mkazi wa Ilomba 
jijini Mbeya.
Makabidhiano ya Cherehani hiyo yalifanyika hivi karibuni Ikulu jijini Mbeya.
Akimkabidhi cherehani hiyo Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa WAMA
 alisema kuwa moja ya kazi anazozifanya ni kumuinua mwanamke kiuchumi 
hivyo basi alitoa  cherehani hiyo ili iweze kumsaidia mjane huyo katika 
maisha yake.
Mama Kikwete alisema kuwa  cherehani hiyo ni moja ya vyerehani 
walivyovipata kutoka nchini  China kwani  watu wanapoomba kusaidiwa siyo
 kama vitu wanavyovihitaji vipo bali nao  wanatafuta sehemu mbalimbali 
 wakipata wanafikisha kwa wahitaji.
“Nakutakia  kila la heri katika kazi zako ila usisahau kuleta mrejesho 
kama kazi inaendelea au la,  isije ikatokea baada ya muda cherehani 
 ikauzwa  hiyo siyo maana yake bali  ifanye kazi ya kuzalisha ili  nawe 
uweze kujiinua kiuchumi”, alisema Mama Kikwete.
Kwa upande wake Fatma Almasi alimshukuru Mama Kikwete kwa msaada 
aliompatia  kwani amekuwa akihitaji kuwa na cherehani ya kudarizi kwa 
kuwa uwezo wa  kudarizi anao lakini hakuwa na kitendea kazi na aliahidi 
kuongeza cherehani kingine kutokana na nguvu zake mwenyewe.
Fatma alisema, “Kinamama tujitahidi  kujikwamua kimaisha kwani mwanamke 
akiwezeshwa anaweza,  tusiwe   wategemezi kwa kina baba  na mtu asijione
 kuwa yeye ni mjane au anaishi na Virusi Vya Ukimwi (VVU)  hawezi 
kufanya jambo lolote na kuona kuwa ni mwisho wa maisha bali ajitahidi 
 kuwa mjasiriamali kwa kufanya hivyo ataweza kukabiliana na hali ngumu 
ya maisha”.
Aliwaomba wanawake kumuunga  mkono na kumtia nguvu Mama Kikwete  kwani 
ana moyo wa huruma na upendo wa kuwasaidia kina mama na watoto wa kike.
Taasisi ya WAMA imekuwa  ikiwainua wanawake kiuchumi, kutoa ufadhili wa 
masomo kwa watoto wa kike ambao hawakupata nafasi ya kusoma, kuimarisha 
afya ya mama wajawazito na watoto na kuwasaidia watoto yatima na 
wanaoishi katika mazingira hatarishi.
 
 
No comments:
Post a Comment