Anna Nkinda – Maelezo, aliyekuwa Mbeya
VIONGOZI  wa Serikali, Dini na Vyama vya Siasa nchini 
wametakiwa kuondoa tofauti zao na kutumia majukwaa kuhubiri amani na 
upendo ili kudumisha mshikamano  na utulivu ndani ya jamii.
Rai hiyo imetolewa hivi karibuni na Mchungaji wa Kanisa la Moravian 
Tanzania Jimbo la Kusini Magharibi Ushirika wa Itiri  Daniel Siame 
wakati wa ibada ya mazishi ya Ditective Sagenti Christopher Kyendesya 
 aliyefariki Juni 19 mwaka huu wilayani Kisarawe mkoani Pwani kwa ajali 
ya Pikipiki.
Mchungaji Siame alisema kuwa Serikali haina dini bali jamii ndiyo 
inadini mbalimbali zikiwemo za Ukristo, Uislamu na Upagani na kuwaomba 
viongozi hao pale wanapokutana na wananchi kuhubiri mambo yanayompendeza
  Mwenyezi Mungu.
“Inawezekana kuwa ndani ya dini zetu kuna watu ambao wanamapokeo ya dini
 tu na siyo kumtangaza Mwenyezi Mungu hivyo basi sisi kama viongozi wa 
Serikali, Dini na Vyama vya siasa tunakazi kubwa ya kutangaza mambo ya 
kumpendeza Mwenyezi Mungu na amani na siyo mambo ya uchochezi”, alisema 
Mchungaji Siame.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro alimshukuru 
mchungaji huyo kwa kuwahimiza watu wote wakiwemo viongozi na wananchi 
kuhusu umuhimu wa amani na upendo katika jamii.
Kandoro alisema kuwa ni jukumu lao viongozi wa Serikali, Dini na 
wanasiasa kutumia lugha ya kuwajenga watanzania ili waone kuwa amani ni 
silaha ya maisha yao ya kila siku kwani ikivurugika msingi mkubwa wa 
maisha unaharibika na hakuna hata mmoja atakayefurahi kuona kuwa amani 
na upendo vinatoweka.
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete ni miongoni mwa viongozi mbalimbali 
waliohudhuria mazishi hayo wakiwemo pia maofisa wa Jeshi la Polisi, 
wanasiasa, wasomi na  watendaji wa Serikali.
 
 
No comments:
Post a Comment