KWA MAWASILIANO ZAIDI: E-mail: yusuf.badi2@gmail.com.

NSSF

TANGAZO

Friday, August 5, 2016

Zijue kazi za wanasheria wa Taasisi ya Manunuzi ya Umma.

Jacquiline Mrisho-MAELEZO.

MOJA kati ya sekta ambazo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amezizungumza sana katika hotuba zake ni sekta ya Manunuzi ya Umma ambayo ameonesha wasiwasi kuwa sekta hiyo ina mianya inayopoteza fedha za Umma.
Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2011 na Kanuni zake imeweka bayana taratibu za kufuata hadi Mkataba kukamilika katika kufanya manunuzi ya Umma.

Katika hatua hiyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali imepewa nguvu kupitia Kifungu cha 60 cha Sheria hiyo na Kanuni ya 59 ya Kanuni za Ununuzi wa Umma za Mwaka 2013.

Katika kusisitiza hilo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Benno Sanga anasema kuwa msingi mkubwa wa sheria hiyo ni ushindanishwaji wa wazabuni unaoweza kuiletea Serikali thamani ya fedha.

“Kila taasisi ya Serikali lazima ifuate Sheria ya Manunuzi ya Umma kwa manunuzi mbalimbali ya vifaa vya ofisi, sheria hii imeweka utaratibu wa kuhakikisha fedha iliyotumiwa inalingana na huduma inayopatikana”,anasema  Sanga.

Hapo awali Kanuni ya 59 ya Kanuni za Ununuzi wa Umma za Mwaka 2013 ilikuwa inaelekeza kwamba mikataba yote ya ununuzi wa umma ambayo thamani yake inafikia shilingi milioni hamsini au zaidi ifanyiwe uhakiki na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kabla ya kusainiwa lakini kwa sasa kanuni hizo zimerekebishwa kupitia Marekebisho ya Kanuni za Ununuzi wa Umma za Mwaka 2016 na sasa mikataba ya ununuzi ambayo inatakiwa kuhakikiwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa mujibu wa Kanuni 59(1) ya Kanuni hizo ni ile yenye thamani ya kuanzia shilingi bilioni moja au zaidi na mikataba ya ununuzi inayohusu ushindani wa zabuni ya kimataifa.

Kwa mujibu wa Kanuni ya 59(2) ya Kanuni za Ununuzi wa Umma, mkataba wowote wa aina hiyo ambao haukufanyiwa uhakiki na Mwanasheria Mkuu utakuwa batili.

Aidha, Kanuni ya 59(5) inaelekeza kuwa Afisa Masuhuli anapaswa kuhakikisha kuwa ushauri wa kisheria uliotolewa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati akihakiki mkataba husika umezingatiwa ipasavyo na kuingizwa katika rasimu ya mkataba.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali George Masaju amefafanua kuwa kwa mikataba ambayo iko chini ya thamani ya shilingi bilioni moja inafanyiwa upekuzi na Afisa Sheria wa Taasisi ya Manunuzi husika kama inavyoelezwa katika Kanuni ya 60(1).

”Hata hivyo, kwa mujibu wa Kanuni ya 60(4) ya Kanuni za Ununuzi wa Umma, Taasisi ya Manunuzi haizuiwi kuomba ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa jambo lolote linalohusu mkataba unaoweza kuhakikiwa na Afisa Sheria (Legal Officer) wa taasisi husika”, anasema Masaju.

Divisheni ya mikataba ni moja ya ofisi zilizoko chini ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inayojumuisha wanasheria wa taasisi ya manunuzi ya umma ambayo inashughulikia masuala yote ya kuhakiki mikataba kwa makini ili kufahamu kama  taratibu za manunuzi zimefuatwa pamoja  na kutoa ushauri wa mikataba ya manunuzi ya umma kwa taasisi mbalimbali za Serikali.

Divisheni hiyo ya Mikataba ina jukumu la kutoa ushauri wa kisheria kwa taasisi za Serikali kwa uadilifu na uweledi wa hali ya juu, kushiriki majadiliano kwa nia ya kuingia makubaliano na nchi moja au zaidi ya moja.

Pia kushiriki katika kazi mbalimbali za Serikali ambazo zinahitaji muongozo wa kisheria pamoja na upekuzi wa mikataba ihusuyo Serikali ikiwemo ya hati za makubaliano, mikataba ya upangaji, mikopo, madini, mafuta na gesi, ununuzi wa umeme, utekelezaji wa miradi, mikataba itokanayo na zabuni.

Jukumu lingine ni kuangalia ibara mbalimbali za mkataba kama zimewekwa sahihi ili kuondoa uwezekano wa athari hasi kwa Serikali na kujiridhisha kama mikataba husika inakidhi au kuzingatia maslahi ya Umma au Taifa.

Hata hivyo, “chochote kizuri huwa hakikosi kasoro”, majukumu hayo yanaingiwa na changamoto nyingi kwa kuwa Divisheni ya Mikataba iko katika Makao Makuu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pekee.

Hivyo, mikataba hiyo imekuwa ikipelekwa Dar es Salaam kwa ajili ya kuhakikiwa, hatua ambayo imekuwa ikisababisha wadau wa masuala hayo hasa Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa, Jiji na wengine walioko mikoani kusafiri na kupeleka mikataba Dar es Salaam kwa ajili ya uhakiki. Mbali na kuongeza gharama kwa halmashauri na wadau wengine, utaratibu huo unaweza kuchelewesha mradi kuanza mapema.

Kutokana na changamoto hiyo, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inaona umuhimu wa kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali waliopo katika ofisi zao za Mikoani ili baadhi ya Mikataba iwe inahakikiwa na ofisi hizo.

Akifungua semina ya mafunzo ya Mawakili wa Serikali yanayohusu Sheria ya Manunuzi ya Umma, Mwanasheria Mkuu wa Serikali George Masaju anasema kuwa "Kutokana na changamoto hiyo, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inaona umuhimu wa kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali wa Ofisi za Mwanasheria Mkuu wa Serikali zilizoko mikoani ili hatimaye baadhi ya mikataba kutoka kwa wadau walioko wilayani na mikoani iwe inapelekwa katika Ofisi za Mwanasheria Mkuu wa Serikali zilizoko mikoani".

Masaju anaongeza kuwa kutokana na kuongezeka kwa thamani ya mikataba inayohakikiwa na Wanasheria wa Taasisi ya Manunuzi ni wazi kwamba wanasheria hao wanatakiwa kujengewa uwezo kuhusu uhakiki wa mikataba kwani iwapo watashindwa kutekeleza wajibu huo ipasavyo watawajibishwa kwa kuchukuliwa hatua stahiki za kinidhamu au kisheria.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Mikataba (Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali) Bi.Monica Otaru anasema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia mawakili kufanya upekuzi wa mikataba kwa makini na uhakika zaidi.

“Pamoja na kuwa kazi ya kupekua mikataba ni sehemu ndogo ya kazi zetu lakini inachukua muda mwingi, hivyo mafunzo haya yatawaandaa Mawakili wa Serikali walioko katika Ofisi za Kanda kuweza kufanya upekuzi wa mikataba kwa umakini na uhakika zaidi”,alisema Bi. Otaru.

Ili Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itekeleze wajibu huo wa kuhakiki mikataba kwa ufanisi ipasavyo, Wizara, Taasisi na Idara za Serikali zinazopeleka Mikataba katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali zinakumbushwa kuzingatia mambo ya msingi.

Mambo hayo ni masharti ya kifungu cha 22 cha Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, 2005, Kanuni ya 13(1) ya Kanuni za Utekelezaji wa Majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya mwaka 2006 inayoelekeza namna ya kupata ushauri katika Ofisi hiyo kwa kuainisha maelezo muhimu kuhusu mkataba husika.

Pia kuandika barua ya kuiomba Ofisi kuhakiki mkataba husika ili Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itoe ushauri wake ikiwa inaelewa vizuri yaliyomo katika mkataba husika.

Wakati wa mafunzo hayo, Wakili wa Serikali Mwandamizi Divisheni ya Mikataba, Said Kalunde anaelezea juu ya mambo muhimu ya kuzingatia katika kufanya upekuzi wa mikataba ya ununuzi  ikiwemo ya ujazaji wa fomu mbalimbali zinazotumika katika uhakiki wa mikataba hiyo kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya Umma.

“Ni muhimu sana kwa wakili kujiridhisha kama taratibu za ujazaji wa fomu zimefuatwa na fomu zimejazwa kwa usahihi, endapo wakili hatojiridhisha kwa kuhakiki fomu hizo huenda akapatwa na matatizo makubwa ya kiutendaji”,alisema Kalunde.

“Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inapenda kuzikumbusha Wizara, Idara na Taasisi za Serikali kuzingatia ipasavyo masharti ya kifungu cha 20(1) cha Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali cha mwaka 2005 kinachoelezea kuhusu mambo muhimu ya kuzingatia pale wizara na taasisi zinapohitaji huduma za kisheria kutoka nje ya Ofisi ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.”anasema Kalunde.

Anafafanua kuwa kifungu hicho kinaelekeza kuwa," Mkataba wa utoaji huduma ya kisheria kwa Wizara au Taasisi ya Serikali uingiwe baada ya kupata kibali kwa maandishi kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali".

No comments: