KWA MAWASILIANO ZAIDI: E-mail: yusuf.badi2@gmail.com.

NSSF

TANGAZO

Tuesday, January 29, 2013

KABANGE TWITE KUSUBIRI MSIMU UJAO YANGA MPO.

Mchezaji Alain Kabange Twite hataweza kuichezea Yanga msimu huu (2012/2013) baada ya klabu hiyo kuingiza nyaraka zenye upungufu wakati ikimuombea Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa njia ya mtandao (Transfer Matching System- TMS).

Kwa mujibu wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), baadhi ya nyaraka zenye upungufu katika maombi hayo ni mkataba kati ya Twite na Yanga, lakini vile vile makubaliano ya mkopo (Loan Agreement) kati ya Yanga na FC Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) ambayo ndiyo inayommiliki mchezaji huyo.

Ili mchezaji aweze kupata ITC kwa njia ya TMS, kwa mujibu wa Kanuni za Uhamisho wa Wachezaji za TFF kuna nyaraka kadhaa muhimu zinatakiwa kukamilika katika maombi hayo ili hati hiyo iweze kupatikana.

AZAM YAIFUKUZIA YANGA VPL
Michuano ya Ligi Kuu ya Vodacom inaingia raundi ya 15 kesho (Januari 30 mwaka huu) kwa mechi mbili ambapo Azam iliyo katika nafasi ya pili nyuma ya Yanga itakuwa mwenyeji wa Toto Africans ya Mwanza.

Mechi hiyo itachezwa Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam huku Azam ikisaka ushindi ili kuikaribia Yanga inayoongoza wakati Toto Africans inayonolewa na John Tegete ikitaka kurekebisha makosa ya kupoteza mechi yake iliyopita dhidi ya Oljoro JKT.

Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Oljoro JKT dhidi ya wageni Kagera Sugar kutoka Bukoba mkoani Kagera itakayochezeshwa na mwamuzi Jacob Adongo wa Musoma.

Ushindi kwa Oljoro JKT yenye pointi 17 utaihakikishia kubaki katika nafasi yake ya nane wakati Kagera Sugar inayofundishwa na kocha mkongwe Abdallah Kibaden utaifanya ipige hatua moja mbele katika msimamo wa ligi.

Ligi itaendelea tena Jumamosi (Februari 2 mwaka huu) kwa mechi tatu ambapo vinara Yanga wataumana na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Polisi Morogoro ikiikaribisha African Lyon mjini Morogoro.

Nazo Mgambo Shooting ya Tanga na Ruvu Shooting ya Mlandizi mkoani Pwani zitaoneshana kazi kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

KAMPUNI TANO ZAOMBA KUKARABATI HOSTELI TFF
Kampuni tano zimewasilisha tenda zao kuomba kupewa kazi ya kukarabati hosteli ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Januari 7 mwaka huu TFF ilitangaza tenda kwa ajili ya ukarabati wa hosteli hiyo baada ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kukubali ombi lake la kutoa fedha kwa ajili ya kazi hiyo.

Ufunguzi wa tenda hizo ulifanyika jana (Januari 28 mwaka huu) kupitia kwa Bodi ya Tenda ya TFF mbele ya wazabuni wote watano waliowasilisha tenda zao na kushuhudiwa pia na Mkandarasi mshauri. Wazabuni (kampuni) waliojitokeza awali walikuwa saba, lakini waliorejesha zabuni zao ni watano.

Kampuni hizo ni Crescent Concrete Limited, DGS Company Limited, Mart Builders Company Limited, Prince General Investment Limited na Send Star Company Limited.

Bodi ya Tenda ya TFF itakutana Januari 31 mwaka huu pamoja na mambo mengine kuchagua kampuni ambayo itafanya ukarabati huo.

LALA SALAMA DARAJA LA KWANZA KUANZA JUMAMOSI
Mzunguko wa pili wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL) ambayo itatoa timu tatu zitakazocheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao (2013/2014) unaanza Jumamosi (Februari 2 mwaka huu) katika viwanja tisa tofauti.

Kundi A litakuwa na mechi kati ya Mbeya City na Burkina Faso itakayochezwa Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, Majimaji na Kurugenzi katika Uwanja wa Majimaji mjini Songea, na Polisi Iringa dhidi ya Mkamba Rangers kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa.

Mechi za Kundi B, Jumamosi (Februari 2 mwaka huu) itakuwa Transit Camp na Ndanda itakayochezwa Uwanja wa Mabatini mkoani Pwani, Moro United dhidi ya Villa Squad (Uwanja wa Karume, Dar es Salaam). Jumapili (Februari 3 mwaka huu) ni Tessema na Green Warriors (Mabatini, Pwani), Ashanti United na Polisi Dar (Uwanja wa Karume, Dar es Salaam).

Kundi C Jumamosi (Februari 2 mwaka huu) ni Polisi Dodoma na Kanembwa JKT (Uwanja wa Jamhuri, Dodoma), Morani dhidi ya Mwadui (Uwanja wa Kiteto, Manyara), Polisi Mara na Pamba (Uwanja wa Karume, Musoma), Polisi Tabora na Rhino Rangers (Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora).

Ligi hiyo inatarajiwa kumalizika mwishoni mwa Machi mwaka huu ambapo mshindi wa kila kundi atapanda daraja kucheza Ligi Kuu msimu ujao. (Ratiba imeambatanishwa)

WAPAMBE MARUFUKU KWENYE PINGAMIZI, USAILI TFF
Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imesema waliowekewa pingamizi na wa walioweka pingamizi hawaruhusiwi kufika katika kikao cha kesho (Januari 30 mwaka huu) wakiwa na vikundi vya ushangiliaji au wapambe.

Kikao cha kupitia pingamizi kitafanyika saa 4 asubuhi na wapambe au washabiki wa waombaji uongozi pamoja na waweka pingamizi hawakiwi kuwepo kwenye eneo la kikao hicho.

Wote walioweka pingamizi na waliowekewa pingamizi barua zao za mwito wa kuhudhuria kikao cha  Kamati ya Uchaguzi ya TFF zimeshatumwa kwenye anwani za barua-pepe zilizo kwenye taarifa za pingamizi au kwenye fomu za maombi ya uongozi.

Leo waombaji uongozi watatumiwa barua za mwito kwa barua-pepe wa kuhudhuria usaili utakaofanyika tarehe 01-02 Februari 2013. Tarehe 01 Februari 2013 watasailiwa waombaji uongozi wa TPL Board na waombaji ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF kupitia Kanda ya 1 hadi Kanda ya 8. Waombaji uongozi kupitia Kanda ya 9 hadi ya 13 na waombaji uongozi wa Makamu wa Rais na Rais wa TFF watasailiwa tarehe 02 Februari 2013 kuanzia saa 4 asubuhi.

Vyombo vingi vya habari vimeonyesha nia ya kuwepo mdahalo wa wagombea uongozi katika TPL Board na TFF. Kanuni za Uchaguzi za TFF hazizuii jambo hilo kufanyika, bali tu lizingatie Kanuni za Uchaguzi za TFF. Mojawapo ya mambo ya kuzingatiwa ni kwamba mdahalo huo ufanyike wakati wa kipindi cha Kampeni na usiwe na taswira ya kuwapendelea au kuwabagua baadhi ya wagombea. Kanuni hazimlazimishi mgombea kushiriki mdahalo.

Pia ni vema mdahalo ukaandaliwa na kuratibiwa  na Taasisi inayounganisha vyombo vya habari au waandishi wa habari kama TASWA. Kamati ya Uchaguzi ya TFF lazima ijulishwe kwa maandishi nia hiyo ya kufanyika mdahalo na utaratibu utakaotumika mapema kabla ya kufanyika mdahalo huo ili kujiridhisha kuwa utaratibu utakaotumika kuandaa na kuendesha mdahalo haukiuki kanuni za Uchaguzi za TFF.

Kamati ya Uchaguzi ya TFF inavishukuru vyombo vya habari kwa kuzingatia Kanuni za Uchaguzi hadi sasa na kuwaomba waendelee kufanya hivyo hadi mwisho wa mchakato wa uchaguzi.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments: