KWA MAWASILIANO ZAIDI: E-mail: yusuf.badi2@gmail.com.

NSSF

TANGAZO

Wednesday, November 11, 2015

ASASI YA FORUM CC TANZANIA YAMWAMBIA RAIS NA UONGOZI UNAOTARAJIWA KUHUSU HATUA ZA KUCHUKUA DHIDI YA ATHARI ZA MABADILIKO YA TABIA NCHI.

 Mwenyekiti wa Forum CC Asasi Mwavuli wa Kitaifa wa Asasi za Kiraia zinazoshughulika na kupunguza athari za mabadiliko ya Tabianchi,Euster Kibona (katikati) akizungumza na waandishi kuhusu kumuomba rais kuchukua hatua dhidi ya athari za mabadiliko ya tabia nchi  Dar es Salaam jana. Mwengine ni  Mshauri Mwelekezi Beatrice Kamugisha (kushoto) na Ofisa Mipango Fazal Issa.
 Ofisa Mipango wa ForumCC, Fazal Issa (kushoto)
Mwenyekiti wa Forum CC Asasi Mwavuli wa Kitaifa wa Asasi za Kiraia zinazoshughulika na kupunguza athari za mabadiliko ya Tabianchi,Euster Kibona (kushoto) akizungumza na waandishi kuhusu kumuomba rais kuchukua hatua dhidi ya athari za mabadiliko ya tabia nchi  Dar es Salaam.Mwengine ni Ofisa Mipango Fazal Issa.


Dar es Salaam, Novemba 11, 2015 - 
 ForumCC ni asasi mwamvuli wa kitaifa wa asasi za kiraia zinazoshughulika na kupunguza athari za  Mabadiliko ya Tabianchi kwa kushirikiana na  wanachama wake. Kipekee tunachukua fursa hii kutoa pongezi zetu za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania - John Pombe Magufuli; Wabunge na Madiwani wote kwa kuweza kupata ridhaa ya Watanzania kuongoza serikali ya awamu ya tano.
Tunachukua fursa hii kuwajulisha kuwa tuna matarajio ya juu kutoka kwao kuwa watatimiza ahadi walizotoa kwa Watanzania. Hii ikiwemo kushughulikia athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi ambazo hazijashughulikiwa kwa umakini  kwa muda mrefu sasa.
Mabadiliko ya tabianchi yamekuwa changamoto kubwa ya maendeleo kwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania. Athari zake  zikiwemo kuongezeka kwa joto; ukame; mafuriko; njaa,  ongezeko kubwa la wadudu waharibifu wa mimea, na magonjwa ya mifugo na binadamu; kukauka kwa vyanzo vya maji; kuyeyuka kwa theluji ya Mlima Kilimanjaro na mingine; kuzama kwa visiwa muhimu kwa wavuvi kama  Fungu la Nyani na Maziwe; kuongezeka kwa kina cha bahari; mmonyoko wa fukwe; maji chumvi kuingia katika nchi kavu. Hivi vyote vina athari kubwa sana katika uchumi, usalama wa maisha ya Watanzania kwa ujumla.
Hivyo, tunapenda kutoa maombi yetu yafuatayo kwa Mheshimiwa Rais na uongozi wake:
1.      Madhara ya mabadiliko ya tabianchi ni zaidi ya uharibifu wa mazingira – ni suala la kiuchumi na kiusalama pia: kwa muda mrefu sasa suala la mabadiliko ya tabia nchi zimekuwa zikiwekwa kama suala la kimazingira pekee na hii imekuwa kikwazo kikubwa katika kupambana na changamoto hii. Suala la mabadiliko ya tabianchi liwekwe kama suala la kiuchumi hususani kwa nchi yetu ambayo uchumi wake unategemea sana maliasili (kama ardhi, mvua na misitu). Uchumi wa jamii za kitanzania  umekuwa ukiathirika sana katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, mifugo, maji, miundombinu na nishati. Hali ambayo inaongeza umasikini kwa jamii kwa kasi kubwa sana.
2.      Kuweka jitihada za dhati katika upatikanaji na ukusanyaji wa fedha za maendeleo: ili kuhakikisha mipango na mikakati ya kimaendeleo ya kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kuboresha uchumi; jitihada za dhati zinahitajika kufanyika kwa  Serikali katika upatikanaji na ukusanyaji wa fedha za miradi ya maendeleo kwa ngazi zote. Hii ikiwemo kuziba mianya ya rushwa na ubadhilifu; na pia kuongeza uwezo wa wahusika katika kubuni njia mbalimbali za upatikanaji wa pato la Serikali kitaifa na ngazi ya Serikali za Mitaa.
Kuweka mfumo madhubuti wa kufuatilia upatikanaji na matumizi ya fedha za kupambana na athari za  mabadiliko ya tabianchi zinazopatikana kwa vyanzo vya ndani na jumuiya ya kimataifa ambavyo ni vingi zaidi. Kwa sasa  nchi yetu haina mfumo mahususi wa ufuatiliaji wa vyanzo  hivyo  hususani katika bajeti ya taifa. Hivyo, tunasisitiza kuwe na  mfumo mahususi na madhubuti wa ufuatiliaji ikiwemo kuweka “Code” maalum ya mabadiliko ya tabianchi katika bajeti. Hii itasaidia kuboresha uwazi, uwajibikaji na pia kuvutia wahisani na uwekezaji katika eneo hilo.
Kuhakikisha bajeti ya kilimo inakuwa zaidi ya 10% ya bajeti yote kwa mwaka kama inavyoagizwa na mkataba wa Maputo na Malabo 2014 ambapo Tanzania iliridhia. Bajeti hiyo itolewe kwa wakati na ifike kwa walengwa ambao ni wakulima wadogo wadogo ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ikiwemo upatikanaji wa mbegu bora, wataalam, miundombinu ya umwagiliaji wa teknolojia ya matone.
3.      Usimamizi wa kikamilifu na uratibu katika utekelezaji wa mipango, mikakati na miradi ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi: Tunatoa rai kwa Mheshimiwa Waziri husika kushughulikia kikamilifu swala la mabadiliko ya tabianchi ambalo lipo chini ya ofisi yake kwa kuimarisha uratibu na utendaji wa taasisi zote zenye jukumu la kushughulikia athari za mabadiliko ya tabianchi;
4.      Kuimarisha miundombinu na uhifadhi wa taka ngumu katika miji mikubwa ili kuhakikisha mafuriko hayaleti madhara katika shughuli za kiuchumi na ustawi wa jamii;
5.      Kuboresha mfumo wa ushirikishwaji wa kikamilifu wa wadau na wananchi kiujumla katika mipango na utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayohusiana na mabadiliko ya tabianchi.

Imetolewa na:
ForumCC
S.L.P 105270 - Dar es Salaam
+255 759/658 266 326


No comments: