KWA MAWASILIANO ZAIDI: E-mail: yusuf.badi2@gmail.com.

NSSF

TANGAZO

Friday, December 21, 2012

SACCOS ZATAKIWA KUWAHIMIZA WANACHAMA VIJANA KUJISHUGHULISHA NA KAZI ZA KILIMO- DK,MUKANGARA.

Na Anna Nkinda – Maelezo, Mwanza
Vyama vya Kuweka Akiba na Kukopa (SACCOS) zimetakiwa kuwahimiza  wanachama wao hasa  vijana waliopo ndani ya vikundi vyao kuitumia mikopo wanayoipata katika shughuli  za kilimo cha chakula, ufugaji wa samaki na uvuvi ili kuisaidia nchi kuepukana na tatizo la njaa kwani vijana ni nguvu kazi ya taifa.
Wito huo umetolewa leo jijini Mwanza na  Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dk. Fenella Mukangara  wakati alipozitembelea SACCOS za Mwanza na Wafanyabiashara Wadogowadogo Mkoa  wa Mwanza (WADOKI) ambazo  zilizopata pesa za mkopo kutoka mfuko wa Maendeleo ya Vijana kupitia Halmashauri ya jiji.
Dk. Mukangara alisema kuwa Wizara yake kupitia Halmshauri za wilaya itahakikisha kuwa mashamba yanapatikana ili vijana waweze kujihusisha na kazi za kilimo jambo litakaloifanya nchi kuwa na uhakika wa kupata chakula cha kutosha kwani ni aibu kwa taifa kukumbwa na njaa wakati  kuna vijana wengi wanazunguka mitaani kwa kigezo kuwa hawana  kazi za kufanya.
“Ardhi ipo ya kutosha  ni kiasi cha SACCOS kuamua kuwa hivi sasa vijana watakaochukua mkopo watatumia fedha hizo katika kazi za kilimo, uvuvi na ufugaji wa samaki tunafahamu kuwa shughuli hizi zinahitaji  pembejeo  Wizara yangu   kupitia Idara ya vijana itashirikiana na kusaidiana nanyi kwa kuwa  SACCOS zenu zinawalenga vijana hivyo basi tumieni fursa zinazowazuguka”, alisema Dk. Mukangara.
Kwa upande wa ulipaji madeni ya mikopo kwa wanachama, Dk. Mukangara alizitaka SACCOS hizo kuwajengea wanachama wao hasa vijana tabia ya kulipa mikopo kwa wakati na kuwahimiza  kulipa kodi wanazotakiwa kulipa  kwa kufanya hivyo wawatambua kuwa huduma wanazozipata kutoka Serikalini zinatokana na kodi yao wenyewe.
 
Akisoma taarifa ya WADOKI SACCOS Deograthias Peter ambaye ni Meneja alisema kuwa  hivi sasa wanawanachama vijana 550 kati ya hao wanawake ni 335 na wanaume 215 wanaojishughulisha na kazi mbalimbali za uzalishaji mali katika harakati za kuondokana na umaskini.
 
“Mkopo wa vijana ulikuwa ni mzuri hasa kwa wale ambao kipato chao ni cha chini. Kupitia mkopo huu tuligundua kuwa  kuna uhitaji mkubwa wa fedha hasa kwa vijana ambao hawana ajira na kama wakiwezeshwa wanaweza wakafanya vizuri na kuinua hali zao za maisha. Kwakuliona hilo  tulianzisha mpango wa kutafuta vikundi vya vijana na hadi sasa wanachama vijana wameweza kujipatia ajira kwa kutumia mikopo wanayoipata kutoka WADOKI na kuinua hali zao za maisha”, alisema Peter.
 
Kwa upande wake Meneja wa Mwanza SACCOS James Nyakiha alisema kuwa fedha za mkopo wa vijana zilizotolewa ni ndogo  kwani vijana ni wengi hivyo fedha hizo hutolewa kwa wanachama wachache hali inayoleta hisia ya baadhi ya wanachama kuwa mkopo umetolewa kwa ubaguzi na muda wa mkopo wa mwaka mmoja mmoja  kwa SACCOS hautoi  fursa kwa  ya kuwahudumia wanachama wengi vijana.
 
SACCOS hizo zilipokea mkopo wa vijana mwaka 2009 kiasi cha shilingi milioni tano kwa kila kikundi toka Idara ya Vijana kupitia Halmashauri ya jiji ambao ulitolewa kwa wanachama vijana 12 kutoka SACCOS ya WADOKI na vijana 21 kutoka SACCOS ya Mwanza ambao wamesharejesha mkopo huo.
 
Waziri huyo alizitembelea SACCOS hizo  ambazo ni baadhi ya SACCOS za mkoa huo zilizopata mkopo wa vijana ili  kuona fedha hizo zimewezaje kuwasaidia   vijana kama kundi na kijana mmojammoja waliopata mkopo huo. Katika Mkoa wa Mwanza jumla ya vikundi 14 vilipata mkopo wa vijana ambapo kila SACCOS ilipata  shilingi milioni tano na kuzifanya fedha zilizotolewa katika mkoa huo kufikia shilingi milioni 70.

No comments: